Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » MUHIMBILI YAFANIKIWA UPANDIKIZAJI WA FIGO

MUHIMBILI YAFANIKIWA UPANDIKIZAJI WA FIGO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 Imeandikwa na Sophia Mwambe
HOSPITALI ya Taifa Muhimbili (MNH) wakishirikiana na wataalamu kutoka Hospitali ya BLK ya New Delhi, India kwa mara ya kwanza wamefanikiwa kufanya upasuaji wa kihistoria wa upandikizwaji wa figo.
Upasuaji huo wa kwanza ulifanyika Novemba 21, mwaka huu kwa mwanamke mwenye umri wa miaka 29 ambaye amepatiwa figo na ndugu yake na alikuwa katika hatua ya tano ya ugonjwa huo.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alisema, upasuaji huo wa kihistoria ni kielelezo cha juhudi za serikali ya Awamu ya Tano za kuboresha huduma za afya nchini zikiwemo zile za ubingwa wa daraja la juu.
“Upasuaji huu ni juhudi zinazofanywa na serikali za kupunguza rufaa za wagonjwa wanaohitaji huduma hizo nje ya nchi na hivyo itaokoa fedha ambazo zingelipwa nje ya nchi kugharamia matibabu hayo na badala yake fedha hizo zitatumika katika maendeleo katika maeneo mengine,” alisema Mwalimu.
Alisema kwa zaidi ya mwaka mmoja hospitali hiyo ilijikita katika kuwekeza katika kuongeza ujuzi wa wataalamu wa aina mbalimbali wakiwemo wataalamu wa upasuaji wa kupandikiza figo ambapo wataalamu 19 walipelekwa nchini India kwa mafunzo ya vitendo na wataalamu wawili walipelekwa nchini Norway.
“Utolewaji wa huduma hii hapa nchini utawezesha kwa kiwango kikubwa kupunguza gharama kwa serikali kupeleka wagonjwa nje ya nchi kwakuwa inakadiriwa kwamba utayarishaji wa mgonjwa kwa ajili ya matibabu ya upandikizaji wa figo ikiwemo vipimo mbalimbali kwa mpokeaji na mtoaji pamoja na upasuaji utagharimu wastani wa Sh milioni 21 hii ni nafuu sana ukilinganisha na gharama ya Sh milioni 80 mpaka 100 iliyokuwa ikitumiwa na serikali kupeleka mgonjwa mmoja nje ya nchi na kwa mwaka ilikuwa ikipeleka wagonjwa 35,” aliongeza.
Alisema kutokana na ongezeko la wagonjwa figo nchini serikali imeanzisha vituo vya utakasishaji damu katika Hospitali za Bugando, Hospitali ya Rufaa Mbeya, Chuo kikuu cha Dodoma na KCMC kwa hospitali za serikali pia kwa hospitali za binafsi huduma hiyo inatolewa na hospitali ya Kairuki, TMJ, Regency, Agha Khan, Access na Hindu Mandal.
Aidha alisema ili kuhakikisha huduma za upandikizaji wa viungo unaboreshwa wizara yake inaandaa sheria itakayosimamia upandikizaji wa viungo kwa ujumla. “Hapa tumeandaa tu kanuni ili kuwawezesha Muhimbili kufanya huduma hii, lakini sasa tunatengeneza sheria itakayosimamia upandikazi wa viungo kwa ujumla na tulikuwa tunafikiria hata ile ya upandikizaji wa mtoto na tayari nimeshamuagiza Katibu mkuu kuanza mchakato huo,” alisema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji Mtendaji wa MNH, Profesa Lawrence Museru alisema hospitali hiyo kwa sasa ina wagonjwa wa figo 200 ambao wanapata huduma ya kutakatisha damu.
Alisema asilimia 60 ya wagonjwa hao wanahitaji huduma ya upandikizaji wa figo pamoja na usafishaji wa damu hivyo kuanza kwa huduma hii utawezesha wagonjwa kupata huduma hiyo.
“Tunawashukuru sana wenzetu wa BLK kwa kuwezesha huduma hii na leo tumeandika historia Muhimbili na taifa baada ya kuanza kwa upandikizwaji huu ni kitu kikubwa cha kujivunia kwa nchi yetu,” alisema Museru.
Naye Kiongozi wa jopo la madaktari hao kutoka BLK, Dk Sunil Prakash alisema upasuaji huo ni tukio muhimu kwa nchi ya Tanzania ambapo alishauri wizara ya afya kuhakikisha inatunga sheria kuhusu mambo ya upandikizaji wa viungo mbalimbali vitakavyopatikana kutoka kwa watu waliokufa ambavyo vitawekwa kwa watu wenye uhitaji.
CHANZO HABARI LEO 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa