Home » » WATOTO 20 WAFANYIWA UPASUAJI TAASISI YA MOYO YA JK

WATOTO 20 WAFANYIWA UPASUAJI TAASISI YA MOYO YA JK

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 Imeandikwa na Mwandishi Wetu
TAASISI ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Taasisi ya Okoa Moyo wa Mtoto (SACH) ya nchini Israel, wamefanya upasuaji wa bila kufungua kifua (catheterization) kwa watoto 20 wenye matatizo ya moyo.
Upasuaji huo unatumia mtambo wa Cathlab, umefanyika katika kambi maalumu ya matibabu iliyoanza Novemba 23, mwaka huu na kumalizika leo. Matibabu yaliyofanyika ni ya kuziba matundu kwenye moyo na kutanua mishipa ya moyo.
“Katika kambi hii tunatarajia kufanya uchunguzi wa moyo kwa watoto 100 kati ya hao watoto 60 ambao watakuwa na matatizo makubwa watapelekwa Israel kufanyiwa upasuaji wa kufungua kifua mwakani na 40 watatibiwa nchini,” ilieleza taarifa iliyotolewa na JKCI.
“Tumepanga kufanya matibabu kwa watoto 25. Tunaamini hadi kambi itakapomalizika watoto wote hawa watakuwa wamepata matibabu. Watoto 20 waliopata matibabu wengine wameruhusiwa na waliobaki hali zao zinaendelea vizuri na wataruhusiwa pindi afya zao zitakapoimarika,” iliongeza taarifa.
Tangu mwaka 2015, Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete ilianza kushirikiana na Taasisi ya Okoa Moyo wa Mtoto (SACH) ya Israel, na hadi sasa watoto 40 wamefanyiwa upasuaji wa moyo Israel. Gharama za matibabu ya watoto hawa zinagharamiwa na taasisi hiyo ya JKCI. “Tunawashukuru wenzetu hawa wa SACH kwa kuona umuhimu wa kutoa huduma ya matibabu bure kwa watoto wenye matatizo ya moyo.
Watoto waliotibiwa wamepona na wale ambao walikuwa wanafunzi wanaendelea na masomo yao,” iliongeza. Ilisema wakati kambi hiyo ikiendelea, baadhi ya wafanyakazi wa SACH na JKCI walienda Kagera kufuatilia maendeleo ya mtoto Julius Kaijage (12), mwanafunzi wa darasa la nne Shule ya Msingi Green Acres, Bunazi aliyefanyiwa upasuaji wa moyo Israel mwaka 2013.
“Tumekuwa na tabia ya kufuatilia maendeleo ya watoto tunaowafanyia upasuaji hii inatusaidia kufahamu maendeleo yao,” ilieleza taarifa ya JKCI. Taarifa ya JKCI iliongeza kuwa wanatarajia kuwa na kambi nyingine ya matibabu ya moyo kwa watoto na watu wazima itakayoanza leo hadi Desemba mosi, mwaka huu.
“Katika kambi hii ambayo tutashirikiana na wenzetu kutoka Taasisi ya Open Heart International ya nchini Australia tunatarajia kufanya upasuaji wa kufungua kifua kwa watoto 13 na watu wazima 10,” iliongeza taarifa ya JKCI.
Imewaomba wananchi waendeleee kuchangia damu kwani wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji wa moyo wanahitaji kuongezewa damu wakati wanapatiwa matibabu. Pia imeeleza kutokana na matibabu ya moyo kuwa ni ya gharama, wamewahimiza wananchi kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ambao utawasaidia kulipa gharama za matibabu pindi watakapougua na kuhitaji kupata matibabu.
Mbali ya hayo, Bodi ya Udhamini, uongozi na wafanyakazi wa JKCI wamemshukuru Rais John Magufuli katika hotuba yake aliyoitoa juzi wakati wa ufunguzi wa Hospitali ya Taaluma na Tiba ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili Kampasi ya Mloganzila kwa kuwapatia jengo ambalo watalifanya kuwa jengo la watoto. “Kama mnavyofahamu asilimia 70 ya wagonjwa tunaowafanyia upasuaji wa kufungua kifua ni watoto, tuna vitanda 123 kati ya hivi vitanda vya watoto ni 24 tu,” ilieleza taarifa ya JKCI.
CHANZO HABARI  LEO 

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa