Home » » Madilu: Ninatamani kuondoka mtaani

Madilu: Ninatamani kuondoka mtaani

 
 Dar es Salaam. Wiki iliyopita nilibahatika kuhudhuria Tamasha la Watoto wa Mitaani ambalo liliandaliwa na Shirika la ‘Hope for the Children’ maalumu kwa ajili ya kutafuta vipaji vya uimbaji na uigizaji.
Ilikuwa ni sherehe ya aina yake kati ya zile ambazo nimewahi kuzishuhudia. Kutokana na shauku ya kutaka kujua mengi kutoka kwa watoto hawa kwanza nilivutiwa zaidi na aliyeonekana kuwa mdogo kuliko wote.
Kwa kuwa tamasha hilo lilikuwa linafanyika katika eneo la wazi na kulikuwa na kelele nyingi, nilimwomba mhusika mmoja katika maeneo hayo aniruhusu niingie ukumbini kwa ajili ya kuzungumza na mtoto huyu.
Mtu huyo aliniambia ‘dada ningependa sana kukuruhusu ufanyie mazungumzo humu ndani, lakini hawa watoto hawaamiiki wanaweza kuiba kitu chochote hivyo ninachoweza kukusaidia ni kukupa viti tu, lakini mazungumzo mkafanyie nje’.
Ukiuliza hadithi za watoto wa mitaani kila mtu atakwambia anayoifahamu, zipo za kusikitisha, kufurahisha na kufundisha na hii ni moja kati ya hizo.
Katika maisha ya kawaida inapofika saa 11:00 alfajiri, familia nyingi huanza siku kwa kuamka na kujitayarisha tayari kukabiliana na pilika za siku nzima. Wazazi au wasaidizi wa ndani huwaamsha watoto kwa ajili ya kujiandaa kwenda shuleni.
Watoto huandaliwa kifungua kinywa wakati mwingine hulazimishwa kula ili washibe kwa kuwa shibe ni moja ya nguzo muhimu katika kutafuta elimu.
Kupata elimu, kulindwa, kutotumikishwa na kuthamini ni haki za msingi ambazo watoto wote duniani wanapaswa kuzipata na anapozikosa hizi ndiyo mwanzo wa kuzaliwa kwa watoto wa mitaani.
Nilizungumza na mtoto huyu aitwaye Madilu Ngonyani (12) ambaye katika umri huo pamoja na kuishi mtaani ana jukumu zito la kuitunza familia yake.
Swali la kwanza nililomuuliza ni kwa nini yupo mtaani kwa kuwa katika umri wake alipaswa kuwa shuleni, naye alinijibu akisema hajui kwa nini mpaka wakati huo mjomba wake hajamwanzisha shule ingawa mara kwa mara amekuwa akimpa ahadi hizo.
Ananisimulia sababu ya kuwa pale katika kundi la watoto wa mitaani akisema kuwa baba yake alimwacha kwa mtu ambaye ndiye sasa anayemwambia kuwa ni mjomba wake.
Hakumbuki lini alianza kuishi mitaani isipokuwa anasema baba yake anayemtambulisha kwa jina moja tu la Ngonyani alimwacha kwa mtu huyo akisema anarudi kijijini kwao mkoani Ruvuma kulima.
  
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa