Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Viongozi wengi wanafanya uamuzi wa taifa bila kuzingatia takwimu
sahihi zinazotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu nchini, imeelezwa.
Akizungumza kwenye mkutano wa wahariri Dar es
Salaam jana, Meneja Teknolojia na Masoko wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu
nchini, Mwanaidi Mahiza alisema kuna changamoto kubwa kwa viongozi kwani
wengi wamezoea kuzungumza bila kufuata takwimu sahihi.
Mahiza alisema Ofisi ya Takwimu imejitahidi kuweka
ukaribu wa kutoa taarifa tangu mwaka 2001 ilipoanzisha Tovuti ya
Taarifa za Jamii na Uchumi (TSED), lakini ni watu wachache wanaoitumia
kupata taarifa.
Alisema tovuti hiyo inatokana na ukusanyaji
taarifa za viashiria kutoka idara na taasisi mbalimbali za Serikali,
kutoka vyanzo mbalimbali ikiwamo sensa ya mwaka 1967 hadi 2012, tafiti
na ripoti maalumu.
Akitoa mada, Mchambuzi wa Mifumo ya Kiteknolojia
kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Martin Kimaro alisema faida ya tovuti
hiyo ni utunzaji na uchambuzi wa viashiria kwa makundi yenye mpangilio
maalumu; afya, elimu na kilimo.
Pia, Kimaro alisema tovuti hiyo hutunza viashiria
vya kupima utekelezaji wa Malengo ya Milenia (MDGs), Mpango wa Matokeo
Makubwa Sasa (BRN) na Mkakati wa Kupambana na Kupunguza Umaskini
(Mkukuta).
“Pia, huweza kupima viashiria kwa maudhui
mbalimbali, vipindi maalumu kama elimu kwa wote, ulemavu, umri na
uzee,”alisema Kimaro.
Hata hivyo, Mtaalamu wa Usimamizi Takwimu kutoka
Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (Unicef), Edith Mbatia
alisema kuna changamoto kubwa kuhusu uelewa jinsi ya kutumia takwimu kwa
watu wengi hasa viongozi kwa sababu wengi wanachanganya mambo.
Ofisa Mtakwimu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania
(TRA), Nossor Siriwa alisema kuna haja ya ofisi hiyo kuhakikisha
inaongeza takwimu kwenye tovuti hiyo hasa masuala ya habari, ili
kuwasaidia waandishi wa habari kwenye majukumu ya kila siku.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment