Home » » Wanawake waaswa kujifunza kujiwekea akiba

Wanawake waaswa kujifunza kujiwekea akiba

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Wanawake nchini wameaswa kujenga tabia ya kutunza akiba, ili kufikia malengo wanayojiwekea kwa maendeleo ya familia zao.
Akifungua tamasha la kwanza la wanawake na vijana lililopewa jina la Mwanamke na Akiba mwishoni mwa wiki iliyopita, Mke wa Makamu wa Rais, Asha Bilal alisema tamasha hilo ni fursa ya kupata utaalamu na kupanua wigo wa biashara.
Bilal alisema maendeleo ya Tanzania yanaanza kwa mwanamke kujijengea tabia ya kujiwekea akiba, ambayo ni mkombozi wa baadaye.
“Akiba ni msingi wa maendeleo ya kila mwananchi. Kwa biashara na kila ajira tuliyonayo, bila kuwa na elimu na utaratibu wa kujiwekea akiba tutazidi kuwa na kipato kidogo hivyo kushindwa kujikwamua na umaskini,” alisema Bilal.
Alipongeza Kampuni ya Angels Moment na timu yake kwa kuandaa tamasha hilo la elimu kwa wanawake, hususan waliopo sekta isiyo rasmi kwani linatoa nafasi ya kuwaondoa kwenye utegemezi.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Angels Moment, Naima Malima alisema lengo la tamasha hilo ni kuboresha kasumba ya kujiwekea akiba.
“Tamasha hili limeandaliwa kuwaonyesha wanawake na vijana umuhimu wa kuweka akiba, aina tofauti za kuweka akiba na njia mbalimbali za kuweka akiba na fursa kupitia uwasilishaji mada na maonyesho,” alisema Malima. Alisema washiriki watapata fursa ya kupata elimu kuhusu kukabiliana na hatari ya uhifadhi wa fedha, masuala mbalimbali yanayohusu usimamizi wa fedha.
“Tamasha linatoa fursa za maonyesho na semina ambazo zitawaelimisha wanawake namna tofauti za kuweka akiba, na mbinu mbalimbali za kujikimu,” alisema Bi Naima.
Aliongeza kuwa Tamasha hili pia linakusudia kuwaelimisha wanawake umuhimu wa kuweka akiba, mbinu tofauti za kuweka akiba na jinsi ya kukabiliana na changamoto mbalimbali katika kujiwekea akiba.
Tamasha hilo linalofanyika katika Ukumbi wa Dar Live - Mbagala, jijini Dar es Salaam limehudhuriwa na mamia ya kina mama na vijana ikiwemo wake wa viongozi waliongozwa na Mama Tunu Pinda ambaye ameshiriki kama mjasiriamali wa kuuza mazao ya nyuki.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa