Home » » Ajira Jeshi la Polisi zisitolewe kienyeji

Ajira Jeshi la Polisi zisitolewe kienyeji

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Aprili mwaka uliopita, Jeshi la Polisi lilitangaza kwamba lingerudisha utaratibu wa kuajiri vijana kutoka shuleni ili ‘kukidhi mahitaji ya sasa’ ya jeshi hilo.  

Tumeguswa mno na hatua ya Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam ya kuwafukuza kazi askari wake wanne kwa kushirikiana na majambazi kufanya uhalifu. Askari hao walifukuzwa kazi baada ya kuthibitika kwamba Machi 9, mwaka huu walishirikiana na majambazi 11 kupora kwa kutumia silaha katika ofisi ya Hong Yang inayojihusisha na shughuli za ujenzi na useremala iliyoko Mbezi Beach, jijini Dar es Salaam.
Tunasema tumeguswa mno na hatua hiyo kutokana na jeshi hilo, kwa muda mrefu, limeshindwa kuwang’amua na kuwatimua askari wanaoshirikiana na majambazi kufanya uhalifu, licha ya kelele na malalamiko kutoka kwa wananchi kwamba matukio mengi ya ujambazi yanahusisha baadhi ya askari wa jeshi hilo. Kelele za wananchi pia zimekuwa zikielekezwa kwa jeshi hilo kutokana na askari wake wa ngazi mbalimbali kujihusisha na vitendo vya rushwa.
Tunaunga mkono hatua ya kuwatimua askari hao kwa sababu siyo tu wamefanya uhalifu, bali pia vitendo vyao kwa namna moja ama nyingine vimelidhalilisha Jeshi la Polisi, mbali na kuwakwaza askari ambao ni waadilifu, watiifu na waaminifu wanaotekeleza majukumu yao kikamilifu. Siyo siri kwamba taswira ya jeshi hilo imechafuliwa kwa kiasi kikubwa na askari wake wanaoendekeza tamaa za kupata utajiri wa harakaharaka, huku wakiweka kando viapo vyao na maadili ya kazi yao. Ndio maana wananchi wamechoshwa na vitendo vya askari hao na wanataka kuona wakitimuliwa na kufunguliwa mashtaka.
Tatizo tunaloliona hapa ni mfumo mbovu wa kutoa ajira kwenye jeshi hilo. Utaratibu mzuri uliozoeleka zamani wa kuchuja vijana wakiwa bado shuleni umewekwa kando kwa sababu zisizoeleweka. Badala yake wanaajiriwa vijana bila ya kujua historia yao na wengine wakiwa wa wanatoka kwenye mazingira ya kihalifu. Wengine wanaajiriwa kwa misingi ya rushwa na ‘undugu’, wakati wengine wanaingizwa kwa kuwa watoto wa wakubwa. Hicho ndicho kiini cha kansa inayolitafuna Jeshi la Polisi hivi sasa.
Tuliwahi kushauri kwamba ajira katika jeshi hilo zisitolewe kiholela, bali zitolewe kwa vijana waliofaulu kidato cha sita au wenye shahada za vyuo vikuu waliopata mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT). Hoja yetu ya msingi ilikuwa kwamba vijana wa aina hiyo siyo tu wanakuwa wamepikwa na kufundwa, bali pia wanakuwa wamechunguzwa na kuonekana wana nidhamu inayotakiwa katika majeshi yetu.
Aprili mwaka uliopita, Jeshi la Polisi lilitangaza kwamba lingerudisha utaratibu wa kuajiri vijana kutoka shuleni ili ‘kukidhi mahitaji ya sasa’ ya jeshi hilo. Uamuzi huo ulitokana na jeshi hilo kutambua changamoto zinazolikabili kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, ikiwa ni pamoja na ongezeko la uhalifu mpya kama wizi wa kutumia mtandao, biashara ya dawa za kulevya, usafirishaji haramu wa binadamu na utakasaji wa fedha. Lilitambua pia kwamba sasa wahalifu wanatumia mbinu mpya na utaalamu wa hali ya juu.
Tulilipongeza jeshi hilo kwa kujitambua, lakini tulipendekeza yafanyike maboresho ili kuliwezesha kuwa jeshi la kisasa siyo tu litakaloweza kuvutia vijana wenye ari, weledi, utashi na dhamira ya kufanya kazi za Polisi, bali pia vijana wenye mtazamo na mwelekeo unaoendana na dunia ya sasa. Kinachosubiriwa hadi leo ni utekelezaji wa azma hiyo.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa