Home » » Dk. Gharib Bilal atoa changamoto Chahita, Necta

Dk. Gharib Bilal atoa changamoto Chahita, Necta

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal amekitaka Chama cha Hisabati Tanzania (Chahita) na Baraza la Mitihani Tanzania (Necta) kukaa meza moja ili kuondoa tofauti zilizopo kuhusu namna ya wanafunzi wa darasa la saba kufanya mtihani wa hisabati.
Uamuzi huo umekuja baada ya Necta kuanzisha mfumo wa maswali ya kuchagua katika mtihani wa hisabati, tofauti na ilivyokuwa awali ambapo mwanafunzi alikuwa akikokotoa hesabu hizo. Chahita wanapinga mfumo mpya.
Akizungumza katika maadhimisho ya sherehe ya miaka kumi ya Siku ya Pai (3.14) Tanzania iliyofanyika Dar es Salaam jana, Dk Bilal alisema, wote wawili wanasababu za msingi, kinachotakiwa ni kuangalia wapi kuna makosa.
“Najua ninyi wana mahesabu hampendi maswali ya kuchagua na mna sababu zenu, Necta nao wanasababu zao, hivyo kaeni pamoja mjadiliane ili kumaliza tofauti zilizopo kwa amani kabisa,” alisema Dk Bilal.
Alisema Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) unatakiwa kuonekana kwa vitendo na kwamba utaweza tu kufanikiwa iwapo ushirikiano kati ya jamii na wadau utakuwapo na kuimarishwa kikamilifu.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Chahita, Dk. Sylvester Rugeihyamu alisema wanafunzi wanahitimu darasa la saba na kujiunga na kidato cha kwanza wakiwa hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu kwamba hayo ni matokeo ya kufanya mtihani wa hisabati kwa mfumo wa kuchagua.
“Chama kilikataa mfumo huu wa kuchagua majibu tena kwa somo la hisabati, haifai hata siku moja, hesabu lazima ukokotoe na tunatakiwa kuwajenga wasomi wa nyanja hii sasa kwa njia hii hatuwezi kuwapata,” alisisitiza Dk Rugeihyamu.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa