Home » » Polisi Dar: Tumeshtukia mbinu mpya wauza unga

Polisi Dar: Tumeshtukia mbinu mpya wauza unga

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limedai kubaini mbinu mpya za kusafirisha dawa za kulevya kama cocaine, heroine.
Kamanda wa Polisi wa kanda hiyo, Kamishna Suleiman Kova, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Alisema jeshi hilo limegundua mbinu hiyo baada ya kuwakamata watu wanne kati yao wapo raia watatu wa Nigeria, mmoja Mtanzania, wanaojihusisha kusafirisha dawa hizo.
"Watuhumiwa walikamatwa Machi 18 mwaka huu, katika Ofisi za Kampuni ya DHL, Barabara ya Sam Nujoma, mkabala na Mlimani City, Mwenge wakijiandaa kusafirisha dawa hizo katika kifurushi," alisema.
Aliwataja watuhumiwa kuwa ni Sunday Chaidikaobi (42), Chukwuma Favour (31), Franklin Indubuisi (41) ambao ni raia wa Nigeria na Hadija Ngoma (43), Mtanzania na mkazi wa Kimara Temboni.
 "Watu hawa walikutwa na kifurushi kilichokuwa kikisafirishwa kwenda nchini Liberia, Afrika Magharibi, upekuzi ulifanyika kwa umakini na kubainika kilikuwa na dawa za kulevya.
"Kifurushi hicho kilikuwa na vitabu vitatu vya lugha ya Kiingereza ambavyo katikati ya kurasa za mwanzo na mwisho kulikuwa na unga wa rangi ya kahawia unaoashiria ni heroini," alisema.
Alisema dawa hizo zinakadiriwa kuwa na ujazo wa nusu kilo na uchunguzi zaidi unafanyika ili kubaini thamani, ujazo halisi na aina ya dawa ambapo sampuri yake imepelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwa uchunguzi zaidi.
Wakati huo huo, jeshi hilo linawashikilia watu wawili wenye asili ya Asia wakidaiwa kuhusika na tukio la kuwateka nyara watoto wawili wa kike wa mfanyabiashara wa simu za mkononi katika Mtaa wa Samora, Dar es Salaam, Bw. Aunally Jaffer.
Kamishna Kova, aliyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari na kudai polisi walipata taarifa kuwa kuna mpango wa kuwateka watoto hao Machi 14 mwaka huu.
Mpango huo ulikuwa ufanywe na watuhumiwa Adil Yusuf (24), mkazi wa Kariakoo na Mehul Kava (24), mkazi wa Mtaa wa Jamhuri na Zanaki.
"Lengo la watuhumiwa ni kujipatia fedha sh. milioni 500 baada ya kufanikisha utekaji huo kutoka kwa wazazi wa watoto hawa, ndugu na jamaa zao...hawa watoto ni Shamima Aunally na Halifa Aunally wote wakazi wa Mtaa wa Kisutu na Zanaki," alisema.
Aliongeza kuwa, makachero wa kanda hiyo waliweka mtego na ilipofika Machi 14, saa nane mchana, watuhumiwa walikamatwa wakiwa tayari kuwateka mabinti hao katika eneo la Jet Rumo, Manispaa ya Ilala, kabla ya kutimiza lengo lao.
Kamishna Kova alisema, baada ya kuwahoji watuhumiwa wote walikiri na kudai lengo lilikuwa kupata sh. milioni 500.

Chanzo;Majira


0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa