Home » » Wapinzani wacharuka

Wapinzani wacharuka

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
  Wadai hotuba ya Rais Jk imetangaza kuvunjika kwa Muungano
  Wasema hawako tayari kuona mawazo ya wananchi yakichakachuliwa
Kutoka kushoto: Freeman Mbowe(Chadema), Profesa Ibrahim Lipumba(CUF) na James Mbatia(NCCR - Mageuzi)
 
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), unaoundwa na wajumbe wa vyama vya upinzani walio kwenye  Bunge Maalum la Katiba, umeielezea  hotuba ya Rais Jakaya Kikwete ya uzinduzi wa bunge hilo kuwa imetangaza kuvunjika Muungano.
 
Kadhalika wajumbe hao wamemkosoa Rais kuwa  hakwenda kuzindua bunge hilo  bali kuzindua rasimu ya CCM na kudhalilisha maoni ya wananchi kupitia Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
 
Wawakilishi hao wakichambua hotuba ya Rais walisema hotuba  ya juzi imeonyesha dhahiri kutangaza rasmi kuvunja Muungano baina ya  Tanganyika na Zanzibar.
 
Wakizungumza na wanahabari mjini Dodoma, viongozi wa Ukawa walisema hawako tayari kuona mawazo ya wananchi yakichakachuliwa kwa faida ya chama tawala.
 
Mwenyekiti wa Ukawa, Profesa  Ibrahim Lipumba alisema kuwa katika hotuba yake, Rais Kikwete alitumia muda mwingi kuweka vitisho kuhusu uanzishwaji wa muundo wa serikali tatu kuwa endapo utapitishwa, unaweza kusababisha nchi kupinduliwa na jeshi huku akitoa maelekezo ya kuwapatia Wazanzibar mamlaka zaidi ya kujitawala kama nchi inayojitegemea.
 
Kutokana na kauli hiyo, ni wazi kuwa Zanzibar itajitenga kutokana na yenyewe kuwa na katiba  inayoitambua kama taifa linalojitegemea.
 
“Sisi tulitarajia kwamba Rais atakuja kutuunganisha, badala yake hotuba aliyoitoa ni ya kututenganisha na hatuwezi kukubali kutumiwa kupitisha mambo wanayoyataka CCM badala ya Rasimu ya wananchi iliyowasilishwa na Jaji Warioba,” alisema.
 
 Alisema alichakachua takwimu za Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuhusu watu waliotoa maoni juu ya muundo wa Muungano na alitumia takwimu zilizotolewa kwenye baadhi ya magazeti badala ya takwimu halisi za Tume.
 
 “Tumesikitishwa na kitendo cha Rais kutumia takwimu ‘alizookota’ kwenye gazeti la … (analitaja) na kudhalilisha rasimu ya katiba ambayo yeye mwenyewe alianzisha mchakato wake,” alisema.
 
Alieleza kuwa badala ya kuzindua bunge hilo, alitumia muda mwingi kusisitiza msimamo wa  CCM  kwa kupigia debe rasimu inayodaiwa kuwa tayari imeandaliwa na chama hicho kitu ambacho hakupaswa kukifanya kama Rais wa watu wote.
 
Profesa  Lipumba alisema kama CCM walikuwa na Rasimu yao ya Katiba, walipaswa kuitisha Mkutano Mkuu wa CCM kuijadili na siyo kuipeleka kwenye bunge hilo ambalo ni chombo muhimu cha kujadili mustakabali wa nchi.
 
Alisema hawatakuwa tayari kuona rasimu inayopaswa kujadiliwa ambayo inatokana na maoni ya wananchi inawekwa pembeni na badala yake inaingizwa CCM.
 
Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, James Mbatia alitahadharisha kuwa endapo CCM itaendelea kuchezea mchakato wa katiba mpya itasababisha nchi kuingia kwenye machafuko.
 
Alisema kuwa Rasimu ya Katiba iliyopatikana imetokana na maridhiano ya Wazanzibar ambao waliunda serikali ya kitaifa, hivyo kutokana na matamko ya Rais Kikwete ni dhahiri kuwa amewatukana Watanzania kutokana na mawazo waliyoyatoa kwenye tume.
 
Mbatia alisema Rais Kikwete wakati akipokea rasimu ya kwanza na ya pili pamoja na kwenye mkutano wa maridhiano na vyama vya kisiasa, aliwataka viongozi wa kisiasa kuzingatia maslahi ya nchi badala ya kuweka mbele itikadi zao za kisiasa katika kuhakikisha Tanzania inapata katiba bora.
 
Lakini cha kusikitisha ni kwamba Rais Kikwete mwenyewe amekiuka makubaliano hayo na kuingiza itikadi yake kwa kutetea hadharani msimamo wa CCM na kupuuza maoni ya wananchi. 
 
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chadema Freeman  Mbowe alisema kutokana na hotuba yake, Rais Kikwete ameweka misingi mibaya ya upatikanaji wa katiba nzuri kwa kubeza maoni ya Watanzania.
 
Mbowe alitolea mfano kwa Mwanasheria Mkuu Mstaafu wa Kenya, Seneta Amos Wako aliyesema serikali iliingilia na kuchakachua rasimu ya katiba kwa kuingiza vifungu  13 ambavyo  vilisababisha machafuko nchini humo.
 
“Rais na Chama chake cha CCM wasijidanganye kuwa wingi wao utawasaidia kuchakachua rasimu na kupuuza maoni ya wananchi, tutapambana ndani na nje ya bunge ili wananchi waweze kutendewa haki,” alisema Mbowe.
 
Tundu Lissu kwa upande wake alisema  licha ya kanuni walizopitisha kukataza Rais asifanyiwe dhihaka, itabidi kanuni hiyo isitumike kwa kuwa Rais mwenyewe ameanza kuwadhihaki wabunge na wananchi .
CHANZO: NIPASHE 

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa