Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » Halima Mdee amkana Mkono asema hakulishwa sumu

Halima Mdee amkana Mkono asema hakulishwa sumu


Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee.

Dar es Salaam. Siku moja baada ya Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimrod Mkono kusema amelishwa sumu akiwa London, Uingereza, Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee amemtaka kusema ukweli na si kulihadaa Taifa kwa uongo.
Mkono akizungumza na waandishi wa habari juzi kuelezea mwenendo wa afya yake, alisema lengo la kulishwa sumu ilikuwa ni kutaka kuharibu figo zake ndani ya saa 72 kitendo kilichoshindikana.
Mdee aliyekuwa na Mkono katika ziara hiyo alisema: “Hakuna ukweli wowote kwamba alilishwa sumu, nilikuwa naye kule na mazingira aliyoanza kuumwa hadi kupona kwake ni utata... awaeleze Watanzania anaumwa nini na si kusema alilishwa sumu.
“Nilikaa kimya baada ya kuripotiwa na gazeti moja (The Citizen) kwamba Mkono kalishwa sumu, sasa amezungumza tena nikaona si busara kukaa kimya wakati alilidanganya Taifa. Mkono waeleze ukweli watu mbona unawadanganya.”
Mdee aliwataja baadhi ya wajumbe wa msafara huo wa watu 11 kuwa ni William Ngeleja (Mwenyekiti wa kamati hiyo), Mkurugenzi wa Kupambana na Kuzuia Rushwa Tanzania (Takukuru), Dk Edward Hoseah, Mbunge wa Temeke, Abbas Mtemvu na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika.
“Dk Hoseah ndiye aliyezungumza na daktari wa Mkono kwa kina zaidi na alimweleza kuwa ampatie dawa fulani, sasa kama kweli alilishwa sumu daktari wake alijuaje kuwa sumu hiyo inaondolewa na dawa hiyo aliyomwambia Hoseah ampe.
“Kama ni kutaka kutumia kivuli cha sakata la escrow, arudi bungeni tuijadili na tuimalize ila asiseme kuwa sijui wanataka kumuua ni uongo,” alisema Mdee.
Kuhusu vitisho alivyodai Mkono kutumiwa kabla ya safari hiyo, Mdee alisema: “Kama kweli ni vitisho iweje tulivyokwenda aliamua kulala peke yake, wewe upo safarini na wenzako halafu ukatishwa kuuawa utakwenda kulala peke yako au utalala na wenzako?”
Mkono alisema anaendelea vizuri na anasubiri kujua hatima ya uchunguzi unaoendelea ili kubaini chanzo cha kulishwa sumu.
“Niko vizuri na afya njema... kama kuna mtu anawinda jimbo langu, mwambieni ameshindwa na wananchi wangu nawaeleza kuwa niko salama wasiwe na hofu. Ninataka kujua nani kanilisha sumu na kwa nini?
“Tukiwa uwanja wa ndege nilipokea ujumbe mfupi wa maandishi (hakutaka kuuweka wazi kwa sababu upelelezi haujakamilika), ukinitahadharisha kuwa makini, ujumbe ule ulinishtua kwa kweli,”alisema.
Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa