Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee.
Dar es Salaam. Siku
moja baada ya Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimrod Mkono kusema
amelishwa sumu akiwa London, Uingereza, Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima
Mdee amemtaka kusema ukweli na si kulihadaa Taifa kwa uongo.
Mkono akizungumza na waandishi wa habari juzi kuelezea mwenendo wa afya
yake, alisema lengo la kulishwa sumu ilikuwa ni kutaka kuharibu figo
zake ndani ya saa 72 kitendo kilichoshindikana.
Mdee aliyekuwa na Mkono katika ziara hiyo alisema: “Hakuna ukweli wowote
kwamba alilishwa sumu, nilikuwa naye kule na mazingira aliyoanza kuumwa
hadi kupona kwake ni utata... awaeleze Watanzania anaumwa nini na si
kusema alilishwa sumu.
“Nilikaa kimya baada ya kuripotiwa na gazeti moja (The Citizen) kwamba
Mkono kalishwa sumu, sasa amezungumza tena nikaona si busara kukaa kimya
wakati alilidanganya Taifa. Mkono waeleze ukweli watu mbona
unawadanganya.”
Mdee aliwataja baadhi ya wajumbe wa msafara huo wa watu 11 kuwa ni
William Ngeleja (Mwenyekiti wa kamati hiyo), Mkurugenzi wa Kupambana na
Kuzuia Rushwa Tanzania (Takukuru), Dk Edward Hoseah, Mbunge wa Temeke,
Abbas Mtemvu na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George
Mkuchika.
“Dk Hoseah ndiye aliyezungumza na daktari wa Mkono kwa kina zaidi na
alimweleza kuwa ampatie dawa fulani, sasa kama kweli alilishwa sumu
daktari wake alijuaje kuwa sumu hiyo inaondolewa na dawa hiyo
aliyomwambia Hoseah ampe.
“Kama ni kutaka kutumia kivuli cha sakata la escrow, arudi bungeni
tuijadili na tuimalize ila asiseme kuwa sijui wanataka kumuua ni uongo,”
alisema Mdee.
Kuhusu vitisho alivyodai Mkono kutumiwa kabla ya safari hiyo, Mdee
alisema: “Kama kweli ni vitisho iweje tulivyokwenda aliamua kulala peke
yake, wewe upo safarini na wenzako halafu ukatishwa kuuawa utakwenda
kulala peke yako au utalala na wenzako?”
Mkono alisema anaendelea vizuri na anasubiri kujua hatima ya uchunguzi unaoendelea ili kubaini chanzo cha kulishwa sumu.
“Niko vizuri na afya njema... kama kuna mtu anawinda jimbo langu,
mwambieni ameshindwa na wananchi wangu nawaeleza kuwa niko salama wasiwe
na hofu. Ninataka kujua nani kanilisha sumu na kwa nini?
“Tukiwa uwanja wa ndege nilipokea ujumbe mfupi wa maandishi (hakutaka
kuuweka wazi kwa sababu upelelezi haujakamilika), ukinitahadharisha kuwa
makini, ujumbe ule ulinishtua kwa kweli,”alisema.
Mwananchi
0 comments:
Post a Comment