Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa
SERIKALI imesifu kazi nzuri inayofanywa na Bodi ya Usajili wa
Makandarasi nchini (CRB) na imeahidi kutenga miradi mikubwa ya ujenzi na
kuwapa kwa upendeleo makandarasi wazalendo kama hatua ya kuwajengea
uwezo.
Ahadi hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na Waziri
wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa alipokuwa
akifunga mkutano wa siku mbili ulioandaliwa na Bodi ya Makandarasi
(CRB), mkutano ambao awali ulifunguliwa na Rais John Magufuli.
Alisema Serikali ina wajibu wa kuwajengea uwezo makandarasi wazalendo kwa sababu hakuna mgeni atakayekuja kuwasaidia Watanzania.
Aliwataka makandarasi kutumia fursa hiyo kujenga miundombinu imara na
kwa ubora wa hali ya juu ili miradi hiyo iendane na thamani ya fedha
zilizotolewa katika mkataba.
Alisema maono ya serikali ya awamu ya tano ya kujenga miundombinu
bora na imara na hayawezi kufanyika bila kuwa na makandarasi wazalendo
wenye uwezo wa kuitekeleza kwa viwango vya hali ya juu.
Mwenyekiti wa Bodi ya Makandarasi, (CRB), Consolata Ngimbwa, alisema
Bodi haitasita kuwachukulia hatua kali makandarasi ambao watapewa kazi
na kuzifanya chini ya kiwango.
Alisema kila mkandarasi anapaswa kutekeleza mradi wake kama mkataba
baina yake na mteja wake unavyotaka na ahakikishe thamani ya fedha
zilizotolewa kwenye mradi hiyo inaonekana.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mhandisi Joseph
Nyamhanga, alisema ili makandarasi wazalendo waendelee kuaminika lazima
wakamilishe miradi kwa wakati na kwa ubora wa hali ya juu.
“Rais Magufuli anaposema anachukia rushwa huwa hatanii na ndiyo maana
wakati anafungua alikuja na Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, kwa hiyo suala
la rushwa kwenye sekta hii si la mzaha tutapambana nayo kwelikweli,”
alisema Nyamhanga Nyamhanga.
Chanzo Kutoka Habari Leo
0 comments:
Post a Comment