(Jabari/Picha na Benedict Liwenga-WHUSM)
Serikali ya Tanzania na
Japan zimetiliana saini Mkataba wa Dola za Kimarekani 80,234 sawa na shilingi
za Kitanzania milioni 170 zitakazotumika kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja cha mchezo
wa Baseball.
Hafla ya Utiaji saini wa
Mkataba huo umefanywa leo na Balozi wa Japan nchini Mhe. Masaharu Yoshida pamoja
na Mwenyekiti wa Chama cha Baseball Tanzania (TaBSA), Dkt. Ahmed Makata huku ukishuhudiwa na mgeni rasmi katika hafla
hiyo ambaye ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Moses Nnauye.
Akiongea na Waandishi wa
Habari pamoja na wageni waliohudhuria hafla hiyo, Waziri Nape amesema kwamba, Serikali
ya Japan imekua na uhusiano mzuri ambapo nchi hiyo imekuwa ikiisaidia Tanzania
katika miradi mbalimbali ikiwemo sekta ya michezo.
Aidha, Waziri Nape
amemuagiza Mkurugenzi Idara ya Maendeleo ya Michezo wa Wizara ya Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw.Yusuph Singo kuhakikisha kuwa mchezo wa
baseball unasambaa mashuleni ili kuweza kuvumbua vipaji zaidi kwa vijana.
Ameongeza kuwa, Wizara kwa
kushirikiana na Ofisi ya TAMISEMI imetenga jumla ya shule 55 za sekondari kwa
ajili ya michezo mbalimbali nchini.
“Naishukuru Serikali ya Japan
kwa msaada mliotupatia tutahakikisha kwamba mchezo huu wa baseball unasambaa
mashuleni na kupendwa zaidi na vijana wetu”, alisema Mhe. Nape.
Kwa upande wake Balozi wa
Japan nchini Tanzania, Mhe. Masaharu Yoshida amesema kwamba, msaada wa fedha
hizo utasaidia ujenzi wa kiwanja cha mchezo wa baseball katika shule ya
Sekondari ya Azania iliyopo Jijini Dar es Salaam.
Ameongeza kuwa, mradi huo
umekua ni alama ya Japan kwa umoja wao yaani Serikali ya Japan, Wakala wa
Mahusiano ya Kimataifa wa Japan (JICA), Makampuni binafsi ya Japan na Chama cha
Marafiki wa Baseball Afrika (AFAB) katika jitihada zao za pamoja za kupanda
mbegu za mchezo huo Barani Afrika ikiwemo Tanzania.
“Nina imani kuwa, chini ya
nidhamu njema ya Shule ya Sekondari ya Azania na Chama cha Baseball Tanzania,
kiwanja hiki kitatunzwa ili kiweze kuwa urithi wa Taifa na vizazi vijavyo”,
alisema Balozi Yoshida.
Naye Mwenyekiti wa Chama
cha Baseball Tanzania (TaBSA), Dkt. Ahmed Makata ameishukuru Serikali kupitia
Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mchango wake mkubwa inaoutoa
katika kuuendeleza mchezo huo, na kwa upande mwingine ameishukuru Serikali ya
Japan kwa msaada wa ujenzi wa kiwanja cha baseball ambacho kinatarajiwa
kujengwa hapa nchini.
Mchezo wa Baseball Tanzania
ulianzishwa na Wataalam wa Wakala wa Mahusiano ya Kimataifa wa Japan (JICA) ambapo
Wakala huo umekuwa mstari wa mbele katika kuuendeleza mchezo huo kwa kusaidia
katika masuala ya mafunzo pamoja na vifaa na mapema mwezi Machi mwaka huu, JICA
inatarajia kuleta Mtaalam kutoka Japan ambaye atasaidia kutoa mafunzo juu ya
mchezo huo kupitia TaBSA, na kupitia JICA, TaBSA imepata seti 25 za vifaa vya
mchezo huo.
0 comments:
Post a Comment