Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) inafuraha kuutaarifu Umma kuwa Daktari
wake Bingwa wa Magonjwa ya Moyo ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha
Utafiti na Mafunzo Pedro Kisali Pallangyo ameshinda tuzo ya watafiti vijana wa Kiafrika kwa mwaka 2017 (Young African Researchers Awards 2017). Tuzo hiyo imetolewa na Taasisi ya Sayansi na Utafiti ya nchini Misri.
Dkt.
Pallangyo alishinda tuzo hiyo baada ya kufanya utafiti wa kisayansi
katika masuala ya Afya na dawa za binadamu kwa kuandika machapisho 16
katika majarida (Journal) saba ya Kimataifa ya Afya ya nchini Marekani.
Licha
ya kukabidhiwa tuzo hiyo mshindi huyo atapewa zawadi ya dola za
kimarekani 15,000 (zaidi ya milioni 30 za kitanzania), ngao na cheti.
Tuzo hiyo itakabidhiwa mwezi wa nane mwaka huu mjini Cairo na Rais wa Misri Mhe. Abdi El- Fattah Al-Sis.
Tangu
kuanza kutolewa kwa tuzo ya watafiti vijana wa Kiafrika mwaka 2014
Dkt. Pallangyo ni mtanzania wa kwanza kushinda. Mshindi wa mwaka jana
alitoka nchini Ghana.
Imetolewa na:
Anna Nkinda
Msemaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
0 comments:
Post a Comment