Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » DARAJA LA GHOROFA 3 KUPASUA MAJENGO YA TANESCO, MAJI

DARAJA LA GHOROFA 3 KUPASUA MAJENGO YA TANESCO, MAJI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 Imeandikwa na Mwandishi Wetu
Jengo la Tanesco
RAIS John Magufuli ameiagiza Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kuvunja sehemu ya Jengo la Makao Makuu ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na la Wizara ya Maji na Umwagiliaji yaliyopo katika hifadhi ya barabara ili kupisha ujenzi wa miundombinu ya daraja la ghorofa tatu la Ubungo (Ubungo Interchange) jijini Dar es Salaam.
Rais Magufuli ametoa agizo hilo jana baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa daraja la juu la Tazara (Tazara Fly-Over) na Ubungo Interchange muda mfupi baada ya kurejea Dar es Salaam kutoka kijijini kwake Chato mkoani Geita.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu, akikagua maendeleo ya ujenzi wa daraja la Ubungo, Rais Magufuli amemuagiza Meneja wa Tanroads Mkoa wa Dar es Salaam, Ndyamukama Julius kuvunja sehemu ya jengo la Tanesco na la Wizara ya Maji na Umwagiliaji yaliyopo katika eneo la hifadhi ya barabara ili kupisha ujenzi wa miundombinu ya daraja hilo.
“Sheria ya hifadhi ya barabara katika eneo hilo ni mita tisini kila upande kutoka katikati ya barabara hivyo ni lazima sheria hiyo iheshimiwe ili kuharakisha ujenzi wa daraja la ghorofa tatu katika eneo hilo la Ubungo unafanyika bila vikwazo kwani sheria ni msumeno haina budi kuzingatiwa hata na serikali yenyewe,” alisema Rais Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli ameiagiza Tanroads kutangaza zabuni ya ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa 16 kutoka eneo linapoishia daraja la ghorofa tatu katika eneo la Ubungo kwenda Chalinze ili itanuliwe kwa lengo la kurahisisha usafiri katika Jiji la Dar es Salaam.
Rais Magufuli amewataka makandarasi wanaojenga daraja la Tazara na Ubungo kuharakisha ujenzi wa madaraja hayo usiku na mchana ili yamalizike kwa wakati ama kabla ya muda huo katika kurahisisha maendeleo ya kibiashara katika Jiji la Dar es Salaam.
“Dar es Salaam ni jiji la kibiashara, hivyo hakuna budi miundombinu yake ya usafiri iweze kurahisha usafirishaji wa bidhaa mbalimbali kutoka ndani ya jiji na nje ya Jiji la Dar es Salaam,” alisema Rais Magufuli.
Baada ya kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Rais Magufuli akiwa ameongozana na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alikagua ujenzi wa Daraja la Juu Tazara (Tazara Fly-Over).
Mhandisi wa Masuala ya Usalama wa Ujenzi, Richard Baruani alimueleza Rais Magufuli kuwa ujenzi wa Daraja la Tazara umefikia asilimia 64, na linatarajiwa kukamilika Oktoba mwakani. Kwa upande wa Daraja la ghorofa tatu la Ubungo, Mhandisi Mshauri Reginald Kayanga alisema ujenzi wake unatarajiwa kuanza rasmi mwezi ujao.
Machi 20, mwaka huu, Rais Magufuli aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara za juu Ubungo utakaochukua miezi 30 kuanzia sasa hadi Septemba 2019. Mradi utagharimu takribani Sh bilioni 188.71 ukiwa na lengo la kupunguza msongamano wa magari katika barabara za Morogoro, Nelson Mandela na Sam Nujoma.
Fedha za mradi wa ujenzi wa barabara zenye ghorofa tatu, umefadhiliwa na Benki ya Dunia ambayo imetoa zaidi ya Sh bilioni 186.7 kwa ajili ya gharama za usanifu, usimamizi na ujenzi wa mradi wakati serikali ikichangia zaidi ya Sh bilioni 1 kwa ajili huduma nyingine ikiwemo ulipaji fidia wa nyumba zitakazoathiriwa na mradi huo.
Alipozindua ujenzi huo, Dk Magufuli aliitaka Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia Tanroads kumsimamia mkandarasi Kampuni ya China Civil Engineering Construction Cooperation (CCECC) kujenga barabara za viwango pamoja na kukamilisha ujenzi wake haraka.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa