Home » » TSN YAMPOTEZA MWANDISHI MAHIRI

TSN YAMPOTEZA MWANDISHI MAHIRI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
 Imeandikwa na Mwandishi Wetu
Aliyekuwa mwandishi wa Daily News, Rose Athumani.
TARATIBU za mazishi ya Mwandishi wa Habari wa Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN), Rose Athuman aliyefariki dunia usiku wa kuamkia jana kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili, zinaendelea nyumbani kwa mjomba wake Paul Mushi huko Mbezi, Mpigi Magohe jijini Dar es Salaam.
Familia hiyo ilisema Rose alikuwa akisumbuliwa na homa kali iliyosababisha kifo chake kwenye Hospitali ya Muhimbili alikokuwa amelazwa. Kwa mujibu wa mjomba wa Rose, shughuli za kuaga mwili zitafanyika Jumapili na marehemu atasafirishwa kwao Moshi mkoani Kilimanjaro kwa maziko siku ya Jumatatu.
Ameacha mtoto mmoja wa kiume ambaye yuko kidato cha tatu. Aidha, waandishi wa TSN wamesema kuwa kifo cha mwandishi mwenzao kimeacha pengo miongoni mwa waandishi kutokana na weledi aliokuwa nao katika kazi.
Mwandishi wa habari za michezo wa magazeti ya HabariLeo na SpotiLeo, Rahel Pallangyo alisema kuwa amemfahamu Rose tangu mwaka 2014 na alikuwa mwandishi makini miongoni mwa waandishi wanawake nchini.
“Kwa kweli ni pigo kubwa sana kwangu. Rose alikuwa ni mtu wa watu na rafiki wa kila mtu, lakini kubwa zaidi alipenda sana kazi yake. Hakika TSN imepoteza siyo tu mwanafamilia, bali imepoteza mfanyakazi bora.
Nitamkumbuka kwa ucheshi wake na urafiki wake kwangu,” alisema mwandishi wa gazeti la HabariLeo, Halima Mlacha. Mlacha alisema alifahamiana na Rose tangu mwaka 2003 wakiwa Chuo Kikuu cha Uandishi wa Habari cha Dar es Salaam (SJMC) wakati huo TSJ.
Alisema wakati huo, Rose alikuwa mwaka wa tatu na yeye alikuwa ngazi ya cheti. Alisema baada ya kuachana na Rose chuoni, wakaja kukutana tena kwenye kazi ya uandishi wa habari wakati huo Rose akiwa akifanya kazi na Kampuni ya Magazeti ya Mwananchi upande wa gazeti la The Citizen, kabla ya kuja kujiunga na TSN na kuandikia gazeti la Kiingereza la Daily News.
“Rose alikuwa mwandishi makini. Nilimfahamu tangu Desemba, 2016. Nilipokuja hapa TSN nilianza kutumia kompyuta yake kwa kuwa yeye mwenyewe alikuwa amesafiri kikazi,” alieleza Mhariri Msanifu wa HabariLeo, Geofrey Lutego.
Naye Kaimu Mhariri wa Michezo, Zena Chande alisema kuwa alimfahamu Rose tangu mwaka 2009 alipotokea gazeti la The Citizen. Alisema kuwa Rose alikuwa ni rafiki wa kila mtu na alikuwa na tabasamu muda wote.
Wasifu wa Rose Alizaliwa Septemba 21, 1976 Moshi, mkoani Kilimanjaro. Mwaka 1988-1991 alihitimu masomo yake ya sekondari kwenye Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Matuga iliyopo Mombasa nchini Kenya.
Mwaka 2000-2003 alihitimu Diploma ya Juu ya Uandishi wa Habari kwenye Taasisi ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwezi Julai, 2008 alihitimu mafunzo ya Wataalamu wa Kimataifa wa Uandishi wa Habari kwenye Chuo Kikuu cha Maine, Marekani.
Julai 2002 alifanya mafunzo kwa vitendo kwa miezi minne kwenye gazeti la Majira. Agosti, 2002 hadi Julai, 2004 alifanya kazi Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) kama mwandishi wakati akiwa bado anasoma na baada ya kuhitimu masomo.
Agosti, 2004 hadi Mei, 2009 alifanya kazi na Kampuni ya magazeti ya Mwananchi kama Mwandishi wa habari, Mwandishi wa ripoti maalumu, makala na mratibu wa jarida la elimu.
Kuanzia Agosti, 2009 mpaka mauti yanamkuta, alikuwa akifanya kazi na Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) kama Mwandishi wa habari na makala kwa gazeti la Kiingereza la Daily News.
CHANZO HABARI LEO 

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa