NSSF YAKUTANA NA WAHARIRI NCHINI


*Yatambulisha Skimu ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii ya Sekta Isiyo Rasmi (NISS)

 

*Sasa mwanachama kufungua madai ya mafao kidijitali ‘online’


*Yaweka kipaumbele cha matumizi ya TEHAMA, zaidi ya asilimia 82% sasa zinafanyika kutumia mifumo


* Yatoa Tuzo kwa Vyombo vya Habari vinavyotekeleza vyema sheria ya NSSF, yatambua mchango wa wahariri wastaafu


Na MWANDISHI WETU,

Dar es Salaam. Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Bw. Masha Mshomba ameanika mafanikio mbalimbali ambayo Mfuko umeyafanya yenye lengo la kumuondolea kero mwanachama na kumsogezea huduma huko huko aliko kwa kutumia mifumo ya TEHAMA. Pia ametambulisha Skimu ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii kwa Sekta isiyo rasmi (NISS).


Bw. Mshomba ameeleza mafanikio hayo tarehe 1 Oktoba 2024 wakati akifungua mkutano wa NSSF na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) ulioshirikisha wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari Nchini, uliofanyika katika ukumbi wa NSSF Mafao House Ilala, Dar es Salaam.


Amesema wanaipongeza Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo amekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya NSSF hasa katika miaka minne iliyopita ambapo kumekuwa na ongezeko kubwa la waajiri na wanachama katika Mfuko tofauti na kipindi cha nyuma na kupelekea thamani ya Mfuko kufikia trilioni 8.5 tofauti na trilioni 4.8 wakati alipokuwa anaingia madarakani. 


Bw. Mshomba amesema NSSF inaendelea kuboresha huduma zake kupitia mifumo ya TEHAMA na sasa shughuli nyingi za NSSF zinafanyika kupitia mifumo na kuwa mpaka kufikia mwishoni mwa mwaka huu wa fedha 2024/25, huduma zote muhimu zitatolewa kupitia mifumo, aidha alifafanua ya kwamba kwa sasa zaidi ya asilimia 80 ya shughuli za Mfuko zinafanyika katika Mifumo tofauti na asilimia 42 ya mwaka 2021/22


“Kupitia mifumo ya TEHAMA, NSSF imeweza kuwafikia kwa ukaribu wanachama na wadau wake ambapo kwa sasa hawalazimika kufuata huduma ofisini badala yake wanazipata huko huko waliko na hivyo tumewaondolea adha ya kufuata huduma umbali mrefu,” amesema Bw. Mshomba.


Aidha, amesema NSSF imezindua mfumo unaomuwezesha mwanachama kufungua madai ya mafao kwa njia ya mtandao na kuwa lengo ni kumrahisishia mwanachama kupata huduma karibu zaidi bila ya kufika katika ofisi za NSSF. Pia Mfumo huu utaondoa kabisa usumbufu kama ulikuwepo na pia utawawezesha wanachama wetu tunaowahudumia kupata huduma kwa wakati, kwa kuwa mifumo hii ni wazi na ufuatiliaji unakuwa rahisi.


Kuhusu sekta isiyo rasmi, Bw. Mshomba amesema Mfuko umechukua hatua mbalimbali kuhakikisha wananchi wengi wanahamasika kujiunga na kujiwekea akiba, ambapo kwa sasa unaendelea kutoa elimu kupitia makundi mbalimbali na kuwaeleza faida za kujiwekea akiba kwa maisha ya sasa na ya baadaye.


Aidha, kuanza kwa Skimu ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii kwa Sekta isiyo rasmi (NISS), ni utekelezaji wa mipango mahsusi iliyowekwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) (Millenium Goals) ambayo pamoja na mambo mengine inataka watu wote kuwa kwenye hifadhi ya jamii. Mshomba alifafanua kuwa NSSF imeshaweka mikakati ya kutosha kuwafikia watu wote ikiwa ni kwa makundi na hata mwananchi mmoja mmoja. Wananchi wote watakaojiunga na NSSF watapata Mafao na Huduma mbalimbali kama ambavyo wafanyakazi wengine wote wanapata.

Uwepo wa Skimu ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii kwa Sekta isiyo rasmi (NISS) utatoa fursa ya kuongeza wigo wa Hifadhi ya Jamii kwa makundi ambayo hayanufaiki na huduma hizi ingawa wanashiriki kikamilifu kuchangia uchumi wa nchi, utasaidia juhudi za Serikali za kupunguza umaskini wa kipato kwa wananchi, utaongeza nguvu za uzalishaji mali na kukuza uchumi wa Nchi na mwisho utachochea kasi ya maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Bw. Mshomba amesema pia NSSF ina Skimu ya uchangiaji wa Hiari ambayo inawahusu watumishi wote. “Natumia nafasi hii kuhamasisha na kuwataka mchangie kupitia skimu hii kwa sababu kufanya hivyo mtajikuta mnapata kipato cha ziada, kazi kubwa mbele yetu ni kutoa elimu ili watu wengi wapate uelewa wa jambo hili.” amesema.

Naye, Mwenyekiti wa  Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile amepongeza mafanikio mbalimbali yaliyofikiwa na NSSF hasa katika kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati ukiwemo wa kukamilisha kiwanda cha sukari Mkulazi. Pia amepongeza NSSF kuweka mipango sasa ya kuwafikia wananchi wote walioko katika Sekta isiyo rasmi kwani kwa kufanya hivyo sasa watu wote tutakuwa ni wamoja na hapo baadaye wote tutanufaika, safari ya uzee ni ya kila mmoja wetu na hivyo ni vizuri kila mmoja akifika awe na uhakika wa kesho yake.

Balile alitumia fursa hiyo kuwakumbusha waajiri wa sekta binafsi hasa wamiliki wa vyombo vya habari kuhakikisha wanawasilisha michango ya wafanyakazi wao NSSF kwa wakati ili wanapostaafu waweze kulipa stahiki zao. 

“Leo tumepata bahati tumepata ushuhuda kutoka kwa wastaafu waliokuwa wafanyakazi kutoka katika vyombo vya habari ambao ni wanufaika wa mafao ya kustaafu na pensheni ya kila mwezi Bi. Flora Wingia na Bw. Bakari Machumu” Aidha, wahariri wastaafu wamepewa Tuzo kwa kutambua mchango wao.

Akiwasilisha taarifa ya uendeshaji wa Mfuko, Mkurugenzi wa Uendeshaji, Bw. Omary Mziya amesema NSSF inaendelea kutekeleza majukumu yake ya msingi ambayo ni kuandikisha wanachama kutoka sekta binafsi na sekta isiyo rasmi, kukusanya michango, kuwekeza na kulipa mafao.

Bw. Mziya amesema wanaendelea kutoa elimu juu ya umuhimu wa hifadhi ya jamii ili kuongeza uelewa wa haki ya kujiunga kwenye Skimu ya Hifadhi ya Jamii kwa Sekta isiyo rasmi  (NISS) na kuendelea kuboresha mifumo na kusogeza huduma karibu na jamii.

“Sekta isiyo rasmi ina Watanzania takribani 11 Millioni, hawa wote wanahitaji kinga dhidi ya majanga ambayo ni uzee na majanga mengine yanayoweza kutokea hapa kati, kuachishwa kazi ama kufariki na kadhalika”. 

Sekta isiyo rasmi inatoa nafasi kwa Watanzania wote kujiunga na hifadhi ya jamii, Mwananchi yeyote aliyejiajiri katika sekta isiyo rasmi kama vile kilimo, ufugaji, uvuvi, uchimbaji mdogo wa madini, sanaa mbalimbali, biashara ndogo ndogo, mama lishe/ Baba lishe, bodaboda na wasafirishaji wengine, machinga, wanahabari wa kujitegemea.































"WOMEN IN AVIATION" KUKUTANA OKTOBA 31


Mkurugenzi wa Sheria wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga nchini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake Katika Usafiri wa Anga Tanzania Maria Makalla Memba akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kuzindua shindano la ubunifu wa nembo ya jukwaa hilo kwa wasichana wenye umri kati ya miaka 14 hadi 20 Tanzania nzima pamoja na mkutano wa wanawake viongozi wanaohudumu katika sekta ya usafiri wa anga nchini unaotarajiwa kufanyika siku hiyo ya Oktoba 31 jijini Dar es Salaam.

JUKWAA la Wanawake katika Usafiri wa Anga Tanzania linatarajia kufanya mkutano wake wa kwanza wa viongozi wanawake katika sekta ya usafiri wa anga utakaofanyika tarehe 31 Oktoba 2024 jijini Dar es Salaam mara baada ya kuzinduliwa rasmi mwaka 2023 na Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa maadhimisho ya miaka 20 ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA).

Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi wa Sheria wa TCAA ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake katika Usafiri wa Anga Tanzania, Maria Makalla Memba amesema jukwaa hilo limezindua shindano la ubunifu wa nembo ya jukwaa hilo kwa wasichana wa umri wa miaka 14 hadi 20 Tanzania nzima ambalo mshindi wake atatangazwa Oktoba 31 mwaka huu unaenda sambamba na mkutano wa wanawake viongozi wanaohudumu katika sekta ya usafiri wa anga nchini unaotarajiwa kufanyika siku hiyo ya Oktoba 31 jijini Dar es Salaam.

“Mkutano huu utahusisha marubani, wahandisi wa ndege na mitambo ya ndege, waongoza ndege, wahudumu wa ndege, maafisa usalama katika sekta ya anga na kila mmoja ambaye kwa taaluma yake anahudumia sekta ya anga kwa lengo la kuelezana mafanikio, changamoto, fursa pamoja na tija zilizopo kwenye sekta ya usafiri wa anga”. Amesema Memba

Mkutano huo ambao Jukwaa la Wanawake Katika Usafiri wa Anga litaufanya kwa mara ya kwanza utahusisha wanawake viongozi kwenye sekta hiyo na kufuatiwa na mkutano mwingine utakaohusisha wanataaluma wengi zaidi wakiwemo wenye nafasi za chini kwenye usafiri wa anga hivyo jukwaa hilo linalenga kusisimua jamii hususani wanawake na watoto wa kike kusoma masomo ya sayansi ili kujiunga na sekta hiyo ya anga.

Jukwaa hilo tayari limefungua fursa ya kujiandikisha kwa washiriki wa mkutano huo kupitia kiunganishi cha mtandaoni kilichopo kwenye tovuti ya Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA) huku washindani wa shindano la ubunifu wa nembo ya jukwaa hilo wakitakiwa kuwasilisha kazi zao kupitia anuani ya posta ya mamlaka hiyo.

WATENDAJI VILABU VYA LIGI KUU WANUFAIKA NA ELIMU YA HIFADHI YA JAMII KUTOKA NSSF

*Karia avitaka vilabu vyote ligi kuu kuchangamkia fursa ya kujiwekea akiba

*NSSF waeleza namna  watakavyonufaika kupata mafao, matibabu

Na MWANDISHI WETU,
Dar es Salaam. Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Bw. Wallace Karia amevitaka vilabu vinavyoshiriki ligi kuu Tanzania Bara kuwaandikisha wachezaji, makocha na wafanyakazi wao katika Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) ili waweze kunufaika na mafao mbalimbali yanayotolewa na Mfuko huo ikiwemo matibabu.

Bw. Karia amesema hayo tarehe 14 Agosti 2024 wakati akifungua semina kwa watendaji wakuu wa vilabu vinavyoshiriki ligi kuu, ambayo imeandaliwa na TFF, Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPBL) pamoja na NSSF, iliyofanyika katika ukumbi wa Mafao House Ilala, Dar es Salaam.

Amesema zipo faida nyingi za wachezaji na wadau wengine wa mpira kujiunga na kuchangia NSSF ikiwemo kupata mafao pamoja na huduma za matibabu na wategemezi wao na kuwa jambo hilo litawasaidia kipindi ambacho hawana nguvu za kucheza mpira.

Bw. Karia amevitaka vilabu vyote kuchangamkia fursa hiyo yenye manufaa kwa wachezaji, na kuwa vielekeze nguvu zaidi ya kuandikisha NSSF wachezaji vijana walio chini ya umri wa miaka 20 ili wanapostaafu mpira wanufaike na pensheni ya uzeeni inayotolewa na NSSF.

“Tunawashukuru wenzetu wa NSSF kwa kuja na jambo hili kwetu sisi litatuepusha na zile lawama tulizokuwa tunatupiwa ambazo hazituhusu za wachezaji wa zamani kuishi maisha magumu kwa kukosa kukidhi gharama za matibabu na gharama za maisha, angalau sisi tunaosimamia mpira tutahakikisha wachezaji wanaocheza kipindi hiki wasipate changamoto ambazo wanazipata wenzao,” amesema Bw. Karia.

Naye, Bw. Cosmasi Sasi, Meneja Uandikishaji, Ukaguzi na Michango wa NSSF, amesema kwa mujibu wa mabadiliko ya sheria ya hifadhi ya jamii sura ya 50 ya mwaka 2018, NSSF ndio Mfuko pekee uliopewa jukumu la kuandikisha wanachama waliopo katika sekta rasmi na sekta isiyo rasmi wakiwemo wachezaji wa mpira pamoja na wajasiriamali wengine wote.

“Lengo la NSSF ni kuwafikia wafanyakazi waliopo katika sekta binafsi na tayari kazi hiyo tunaifanya kwa njia mbalimbali, lakini ili tuweze kumfikia kila mmoja tuna jukumu la kutoa elimu ya hifadhi ya jamii, mafao tunayotoa na faida zake. Tunashukuru kupata fursa hii ya kujumuika na wenzetu TFF, TPBL pamoja na watendaji wakuu wa vilabu vinavyoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara kwa lengo la kutoa elimu hii ili waweze kujiunga na kuchangia,” amesema Bw. Sasi.

Amesema wachezaji na watendaji wa vilabu vya mpira ni wadau muhimu ambao wanatakiwa wapate kinga ya hifadhi ya jamii ili waweze kunufaika moja kwa moja kipindi ambacho hawana uwezo wa kucheza mpira kwa kupata mafao yatakayowasaidia kuishi maisha bora uzeeni.

Bw. Sasi amesema sheria ya NSSF imezungumzia mahususi wanaopaswa kujiunga na Mfuko kuwa ni wafanyakazi wote walioajiriwa katika sekta binafsi, raia wa kigeni wanaofanya kazi Tanzania bara, watumishi wa taasisi za kimataifa zinazofanya kazi Tanzania bara na watu waliojiajiri katika sekta isiyo rasmi.

“Tutahakikisha elimu ya hifadhi ya jamii inawafikia wana michezo wote hata waliopo vilabu vya chini, lengo waweze kujiunga na kujiwekea akiba kwa ajili ya kesho yao iliyokuwa njema,” amesema Bw. Sasi.

Naye, Meneja wa NSSF Mkoa wa Temeke, Bw. Ferouz Mtika ameishukuru Bodi ya Ligi, TFF na vilabu vya mpira wa miguu kwa kushiriki semina hiyo yenye lengo la kupata elimu ya hifadhi ya jamii.




NABERERA CTK YAZINDUA MBEGU MPYA ZA NGURUWE TANZANIA


UZALISHAJI wa nguruwe Tanzania umekuwa ukiongezeka kutokana na uboreshwaji wa miradi unaofanywa na wafugaji nchini ambao wamekuwa wakiboresha ili kuendana na soko lililopo kwasasa ambsalo limeonekana kukua.

Ameyasema hayo Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Mifuko, Wizara ya Mifugo na uvuvi, Dk. Stanford Ndibalema wakati wa uzinduzi wa mbegu mpya za nguruwe pamoja na uhimilishaji wa nguruwe kwa njia ya mrija uliofanyika Julai 27,2024 Jijini Dar es Salaam.

Amesema uzinduzi wa mbegu hiyo mpya utasaidia kuongeza kasi ya uzalishaji wa nguruwe nchini na kuweza kukuza soko.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mwendeshaji wa Naberera CTK, Bi Bensolight Msaki amesema kuwa tatizo la mbegu bora za nguruwe Tanzania litapungua sana kutokana na uzalishaji wa mbegu hizi mpya na bora. 

Aidha amesema mbegu hizo mpya zinatarajiwa kuinua hali ya maisha ya watanzania kutokana na uwezo wake mkubwa wa kukua haraka pamoja na kuzaa vibwagala (watoto) wengi na wenye afya.

Nae Mwakilishi kutoka Bodi ya Nyama Bw. Kassimu Mnangwa amewataka wafugaji wa nguruwe nchini kufuata taratibu za ufugaji ikiwa ni pamoja na kupata usajili kutoka Bodi ya Nyama,  ambapo usajili  unafanyika kupitia mfumo wa kielectroniki wa mimis.mifugo.go.tz.

Mbegu mpya za nguruwe zilizozinduliwa ni majike aina ya CG36 na madume aina ya P81 (Pietrain), P26 (Duroc) na P90 kutoka Kampuni ya Choice/Axiom Genetics, Ufaransa.
 
Uzinduzi huo wa mbegu mpya za nguruwe uliambatana na mafunzo juu ya ufugaji na uhimilishaji yaliyoendeshwa na wawezeshaji kutoka Ufaransa, Uganda na Tanzania.














 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa